Usajili Yanga Leo May 22.2018


WACHEZAJI wawili kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), kiungo Cedrick Kabale na mshambuliaji Alain Mulumba wamewasili leo Dar es Salaam kwa ajili ya majaribio ya kusajiliwa na klabu ya Yanga SC.

Wawili hao wameletwa na kocha mpya wa klabu hiyo, Mwinyi Zahera ambaye anataka kuiboresha timu baada ya mapungufu aliyoyaona kikosini. 

Mulumba aliyezaliwa Januari 10, mwaka 1989 anayetokea klabu ya DC Motema Pembe ya Ligi Kuu ya DRC, ijulikanayo kama Linafoot anaweza kucheza nafasi za winga wa kulia na mshambuliaji wa kati, wakati Kabale aliyezaliwa Agosti 2, mwaka 1997 anatokea klabu ya Don Bosco ya Ligi Kuu pia na ana uwezo wa kucheza kama kiungo mchezeshaji na mshambuliaji wa pili. 

Vumi Ley Matampi katika mchezo wa kirafiki DRC na Tanzania Machi 27 Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam Wawili hao wanatarajiwa kuanza mazoezi Alhamisi na watakuwemo kwenye kikosi cha Yanga kitakachoshiriki michuano ya SportPesa Super Cup nchini Kenya mwezi ujao na kama watafanya vizuri watasajiliwa kwa ajili ya mechi nne zilizobaki za Kundi D Kombe la Shirikisho Afrika. 

Pamoja na hao, kocha Zahera anakamilisha mpango wa kumleta kipa wa timu ya taifa ya DRC, Vumi Ley Matampi aliyedaka katika mchezo wa kirafiki na Tanzania Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam Machi 27 mwaka huu Taifa Stars ikishinda 2-0, mabao ya Nahodha Mbwana Samatta na winga Shiza Kichuya. 

Matampi mwenye umri wa miaka 29 amemaliza mkataba wake klabu ya TP Mazembe na habari zinasema amekataa kuongeza ili aende klabu ambayo atakuwa na nafasi ya kudumu kwenye kikosi cha kwanza. 

Wakati huo huo: Kiungo Mkongo wa Yanga, Papy Kabamba Tshishimbi amerejea nchini juzi akitokea kwao, DRC ambako alikwenda kwa ajili ya matibabu baada ya kuumia kwenye mechi dhidi ya Wolaita Ditcha mwezi uliopita nchini Ethiopia. 

Kikosi cha Yanga SC kimerejea jana Dar es Salaam juzi kutoka Shinyanga ambako Jumamosi kilicheza mechi ya tisa bila ushindi kikichapwa 1-0 na Mwadui FC Uwanja wa Kambarage. 

Na jana Yanga wamefanya mazoezi Uwanja wa Chuo cha Maofisa wa Jeshi la Polisi, Kurasini Dar es Salaam kujiandaa na mchezo mwingine wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara leo dhidi ya Mbao FC ya Mwanza.

No comments:

Note: only a member of this blog may post a comment.