Wawili Yanga Warejea Kuelekea Kuwakabili Township Rollers


Kwa muda mrefu Yanga imewakosa wachezaji wake muhimu Donald Ngoma, Thabani Kamusoko na Amissi Tambwe kutokana na majeruhi.

Tambwe alirejea kikosini kwa muda mfupi lakini baadae majeraha ya goti yakamrudisha kitandani.

Ni muda sasa tangu uongozi wa Yanga ubainishe kuwa Kamusoko ameshapona majeraha yake lakini alikuwa haonekani uwanjani kwa kuwa alihitaji muda zaidi ili kuwa fiti.

Habari njema ni kwamba maendeleo ya kiungo huyo yameridhisha benchi la ufundi na sasa upo uwezekano mkubwa Kamusoko akaanza kuitumikia Yanga mapema.

Yeye pamoja na Donald Ngoma wameanza kujifua kikamilifu na kikosi cha Yanga kuashiria kwamba mashine hizo ziko tayari kurejea kuongeza nguvu kuelekea mchezo wa ligi ya mabingwa Jumanne ijayo dhidi ya Township Rollers.

Wakali hawa wanarejea kikosini katika wakati muafaka ambao Yanga ndio imeanza rasmi ligi baada ya kushinda michezo sita mfululizo!

No comments:

Note: only a member of this blog may post a comment.