TFF YAZIPIGA TAFU SIMBA, YANGA CAF



Kikosi cha timu ya Simba.

UONGOZI wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) umesema kuwa unajipanga kuhakikisha unazisaidia timu za Simba na Yanga ili zifanye vizuri katika mechi zake za marudiano za michuano ya kimataifa ambazo zitacheza Machi 17, mwaka huu.



Simba itapambana na Al Masry huko nchini Misri wakati Yanga itavaana na Township Rollers huko nchini Botswana.



Katika mechi hizo Simba ambayo ilitoka sare ya mabao 2-2 na Al Masry hapa nchini inashiriki michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika wakati Yanga ambayo ilifungwa mabao 2-1 na Township Rollers katika mchezo wake wa kwanza, yenyewe inashiriki michuano ya Klabu Bingwa Afrika.



Akizungumza na Championi Jumamosi, Katibu Mkuu wa TFF, Wilfred Kidao, alisema kuwa ili kuhakikisha timu hizo zinasonga mbele katika michuano hiyo wamejipanga vilivyo kuhakikisha wanazisaidia ziweze kutimiza ndoto hiyo.


Kikosi cha timu ya Yanga.

“Tutahakikisha tunazipatia muda wa kutosha wa maandalizi lakini pia tutatuma wawakilishi wetu katika mechi hizo kwa ajili ya kwenda kuweka mambo sawa ili siku zitakapoenda huko zisikumbane na usumbufu.



“Michuano hii ni ya kimataifa na zikifanya vizuri sifa itakuwa siyo kwa klabu pekee bali kwa taifa zima la Tanzania, kwa hiyo inatubidi tushirikiane nazo kwa karibu kabisa ili kuhakikisha zinapata matokeo mazuri katika michezo yake,” alisema Kidao.



Kutokana na hali hiyo, timu hizo hazitacheza tena mechi zao za Ligi Kuu Bara ambazo zilitakiwa kucheza hivi karibuni mpaka hapo zitakapokuwa zimerudiana na timu hizo katika michuano hiyo ya kimataifa.
Usipitwe Na Breaking News Za Soka: Jiunge nasi kupitia Facebook, Bofya LIKE Button...

No comments:

Note: only a member of this blog may post a comment.