Lufunga Hatihati Kuwakosa Lipuli Leo

Mlinzi wa kati wa timu ya Lipuli FC, Novelty Lufunga anaweza asiwe sehemu ya kikosi cha Wana Paluhengo hao kitakacho kutana na Simba leo katika uwanja wa Samora kutokana na kupata maumivu ya mguu.

Lufunga alijiunga na Lipuli mwanzoni mwa msimu huu akitokea Simba alipokuwa hana nafasi mbele ya Wekundu hao kabla ya kugeuka mchezaji muhimu wa timu hiyo kutoka Iringa.

Kocha mkuu wa klabu hiyo, Amri Said 'Jap Stam' amesema kikosi chake kipo kwenye hali nzuri na wachezaji wana morali ya hali juu isipokuwa Lufunga ambaye ana maumivu ya mguu.

Kocha huyo amesema wanafahamu Simba ipo kwenye kiwango bora kwa sasa na ina washambuliaji wenye uchu lakini wamejipanga kuhakikisha wanawazuia na kubaki na pointi zote tatu nyumbani.

"Tunafanya maandalizi ya mwisho wachezaji wapo kwenye hali nzuri isipokuwa Lufunga ambaye ana maumivu ya mguu.

"Tunategemea kupata ushindani mkubwa kutoka Simba ingawa tumejiandaa kuwazima katika uwanja wetu wa nyumbani," alisema mlinzi huyo wa zamani wa timu ya Simba.

Katika mchezo wa kwanza uliofanyika katika uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam timu hizo zilitoka sare ya bao moja.

No comments:

Note: only a member of this blog may post a comment.